Mtanzania anayeishi Afrika Kusini: Yanga inaogopeka Sauzi

Mtanzania anayeishi Afrika Kusini: Yanga inaogopeka Sauzi


Kuelekea katika pambano la Robo Fainali ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika kati ya Yanga SC dhidi ya Mamelodi Sundowns, shabiki wa Yanga SC, Said Saleh anayeishi nchini Afrika Kusini ameichambua mechi hiyo na kusema Yanga SC wanapaswa kuimaliza mechi nyumbani.


Aliongeza kuwa Watanzania wanaoishi nchini humo wameifurahia ratiba hiyo ya kuiona timu yao ya nyumbani ikienda kucheza Afrika Kusini.


“Baada ya ratiba ya robo fainali ya CAFCL kutoka, nilifurahi kuona Young Africans ya Tanzania imepangwa na Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini ambao ni wenyeji wa Pretoria.


“Baada ya ratiba kutoka tu hapa Wasauzi walianza kuogopa wakisema Yanga ni klabu kubwa na ina mashabiki wengi sana Afrika Kusini na wanaamini Yanga itakuwa nyumbani ikija hapa Afrika Kusini.


“Yanga ameingia kwenye hatua ya robo fainali baada ya kufanya vizuri kwenye uwanja wa nyumbani, ninaamini hata mechi ya Yanga na Mamelodi itakayopigwa kwa Mkapa, itaamua mapema abisa nani atakwenda nusu fainali kabla ya mchezo wa pili utakaofanyika hapa Afrika Kusini.


Shabiki huyo aliongeza kuwa Mamelodi ni timu mahiri inapokuwa katika uwanja wao wa nyumbani, hivyo kama Yanga SC wanataka kuitoa timu hiyo wahakikishe wanashinda katika pambano la kwanza litakalochezwa Tanzania.


“Mechi ya kwa Mkapa, Yanga wanatakiwa wajitoe, wacheze kwa moyo, focus yao muda wote inatakiwa iwe kupata ushindi badala ya kuzuia japo kuzuia kwenye soka ni jambo la msingi lakini lengo kuu iwe ni kupata ushindi. Mamelodi ni wazuri sana wakiwa kwao Afrika Kusini.


“Mshabiki wajitokeze kwa wingi kabisa kuwasapoti wachezaji na benchi lao la ufundi. Falsafa za timu hizi kwenye uchezaji wao wote wanafanana, wana makipa wa kisasa. Yanga wahakikishe wanapata ushindi kwa Mkapa kwa sababu mechi itakuwa ngumu sana wakija hapa Sauzi.


“Watumie makosa ya Mamelodi kuwaadhibu, nafasi yoyote ikipatikana kwa washambuliaji, viungo wafunge na wakati huo wasiruhusu kufungwa. “mamelodi ni wajanja kwa mchezaji mmoja mmoja, wote wanaweza kuamua lolote kwenye mchezo. Yanga wajitahidi kutumia vizuri uwanja wa nyumbani ndiyo utawapeleka nusu fainali,” amesema shabiki huyo.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.