Mastaa Simba, Yanga kuitema Stars

Mastaa Simba, Yanga kuitema Stars



Ofisa Habari wa TFF, Cliford Ndimbo, amesema wamepokea barua kutoka kwa klabu hizo mbili na kuridhia maombi yao ya kutaka wachezaji wao kurejea kwenye vikosi vyao mapema kabla ya Machi 24, mwaka huu ili kupata nafasi ya kujiandaa kuelekea katika michezo hiyo ya Robo Fainali.


Simba SC ina wachezaji wanne katika kikosi cha Taifa Stars ambao ni Aishi Manula, Kennedy Juma, Mohamed Hussein Tshabalala’ na Kibu Denis huku Young Africans nayo ikiwa na Aboutwaleb Mshery, Bakari Mwamnyeto, Ibrahim Bacca na Mudathir Yahya.


Akizungumza jijini Dar es salaam, Ndimbo amesema katika utaratibu wa tiketi za kurudi tarehe tofauti na wengine, Simba SC na Young Africans wamekubaliwa wachezaji wao kuruhusiwa mapema baada ya mechi ya dhidi ya Bulgaria watarejea nchini na kujiunga na klabu zao.


“Ni kweli Simba SC na Young Africans zilituandikia barua ya kuomba wachezaji wao ambao wako katika kikosi cha kwanza waliopo kwenye majukumu ya Taifa kujiunga haraka kabla ya Machi 25, mwaka huu, ili kuwahi Programu ya maandalizi ya mchezo wao dhidi ya Al Ahly na Mamelodi Sundowns.”


“Kwa maslahi mapana ya pande zote mbili tumewakubalia, lakini watakuwepo nchini Azerbaijan na kucheza mechi moja dhidi ya Bulgaria baada ya hapo watarejea kuendelea na majukumu ya klabu yao,” amesema msemaji huyo


Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.