Vyuma vinavyoshuka Azam FC, Fei Toto apagawa

  

Vyuma vinavyoshuka Azam FC, Fei Toto apagawa

Kiungo mpya wa Azam FC, Feisal Salum Abdallah ‘Fei Toto’ amesema anajipanga kwa majukumu mapya na anajua kutakuwa na ushindani mkubwa wa namba kutokana na wachezaji wazuri waliopo kwenye kikosi hicho.


Fei Toto, amesema hayo jana wakati wachezaji wa timu hiyo wakifanya vipimo vya afya kwenye Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa ligi.


“Azam FC ina mashindano ya kimataifa, lazima nijipange kuhakikisha nakuwa msaada wa timu yangu kufanya vizuri, leo tupo kwa ajili ya vipimo ili kujua afya zetu kuelekea msimu ujao,” amesema.


Fei ambaye ni mchezaji mpya kwenye uzi wa Azam anasema kipindi ambacho alikaa nje bila kucheza kilimfanya akumbuke kufanya vitu vingi uwanjani anavyoona atavifanyia kazi msimu ujao.


“Kila mchezaji anaweza akapitia kipindi kama changu kwani kufanya mazoezi peke yako hayawezi kufanana na kufanya na timu.


“Nilikuwa nakumbuka kucheza, hivyo ni muda wangu wa kujiandaa kwa sasa, kikubwa wachezaji wenzangu wamenipokea vizuri, hivyo naamini tutafanya kazi kwa ushirikiano kwa ajili ya timu.”


Mbali na hilo, alimzungumzia straika wa Young Africans, Fiston Mayele kwamba anamtakia kila la kheri popote atakapokuwepo, kwani anaheshimu kiwango chake ni cha juu


“Namkubali Mayele ana uwezo mkubwa wa kucheka na nyavu, nilifurahi kucheza naye pamoja Young Africans na ndio maana nimesema abakie Jangwani ama aondoke akawe na majukumu mema kwani hata yeye alinitakia kila la kheri,” amesema.


Fei Toto msimu uliopita alijikuta akiingia kwenye mgogoro mkubwa na Yanga baada ya kuvunja mkataba lakini baadaye walikubaliana na kujiunga na Azam FC.

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.